Thursday, August 13, 2020

OFISI YA INTELIJENSIA YA TAKUKURU KUIMARISHA OPERESHENI ZA KIUCHUNGUZI DHIDI YA VITENDO VYA RUSHWA NCHINI

Na. James K. Mwanamyoto – Dodoma

Tarehe 13 Agosti, 2020.

Kurugenzi ya Intelijensia ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imedhamiria kuimarisha utekelezaji wa operesheni za kiuchunguzi za TAKUKURU dhidi ya vitendo vya rushwa vinavyojitokeza kwa maana ya ufuatiliaji na uchakataji wa taarifa za kiintelijensia zinazopatikana kutoka katika maeneo mbalimbali kwa lengo la kutokomeza vitendo vya rushwa nchini.

Hayo yamesemwa jana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Kapt. (Mst) Mhe. George H. Mkuchika wakati akitoa neno la utangulizi kumkaribisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa kuzindua jengo la Ofisi ya Intelijensia ya TAKUKURU lililojengwa Makao Makuu ya Nchi Dodoma.

Mhe. Mkuchika amefafanua kuwa, jengo hilo ni muhimu sana kwa Serikali ambayo imedhamiria kwa dhati kutokomeza vitendo vya rushwa nchini kwani litatumiwa ipasavyo na watumishi wa Kurugenzi ya Intelijensia ya TAKUKURU kufanya uchunguzi makini, ufuatiliaji wa kina na kuchakata taarifa za kiintelijensia kwa weledi.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Brig. Jenerali John Mbungo wakati akitoa maelezo kuhusu jengo hilo alisema, Kurugenzi ya Intelijensia ni sehemu ya ofisi za Makao Makuu ya TAKUKURU lakini kutokana na unyeti wa kazi zake imetengwa peke yake ili kuiongezea ufanisi kiutendaji.

“Kurugenzi hii ndio inayoshughulika na upatikanaji pamoja na uchakataji wa taarifa mbalimbali zinazosaidia kufanyika kwa operesheni za kiuchunguzi za kuzuia kutokea kwa vitendo vya rushwa nchini”, Brig. Mbungo amefafanua.

Kurugenzi ya Intelijensia ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ilianzishwa mwaka 2018 baada ya muundo mpya wa TAKUKURU kuidhinishwa Novemba 15, 2018 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa akikata utepe kuzindua jengo la Ofisi ya Intelijensia ya TAKUKURU Makao Makuu ya Nchi Dodoma, Agosti 12, 2020. Kushoto kwake ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora, Kapt. (Mst) Mhe. George H. Mkuchika, kulia kwake ni Naibu Waziri, Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Brig. Jenerali John Mbungo.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa akifungua jengo la Ofisi ya Intelijensia ya TAKUKURU Makao Makuu ya Nchi Dodoma, Agosti 12, 2020. Wengine ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora, Kapt. (Mst) Mhe. George H. Mkuchika, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Brig. Jenerali John Mbungo.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa akimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora, Kapt. (Mst) Mhe. George H. Mkuchika alipowasili kwenye jengo la Ofisi ya Intelijensia ya TAKUKURU Makao Makuu ya Nchi Dodoma kwa ajili ya kulizindua. Anayeshuhudia ni Naibu Waziri, Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa akisalimiana na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora, Mhe. Dkt. Mary Mwanjelwa alipowasili kwenye jengo la Ofisi ya Intelijensia ya TAKUKURU Makao Makuu ya Nchi Dodoma kwa ajili ya kulizindua. Anayeshuhudia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utumishi na Utawala Bora, Kapt. (Mst) Mhe. George H. Mkuchika na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Brig. Jenerali John Mbungo (mwenye sare za jeshi).


No comments:

Post a Comment